D.R. CONGO: Rais wa Zamani Joseph Kabila Atajwa Kuwa Mshirika wa Kundi la Waasi la M23
Ripoti mpya ya Kundi la Wataalamu la Umoja wa Mataifa imeonyesha kwa uwazi zaidi kuliko wakati mwingine wowote uwezo wa kijeshi wa muungano wa AFC/M23 pamoja na malengo yake ya kisiasa mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC). Wakati huohuo, ripoti hiyo inaangazia uhusiano unaozidi kuimarika kati ya muungano huo na aliyekuwa Rais wa DRC, Joseph Kabila. Kwa mujibu wa wataalamu hao, uhusiano huo unaweza kuishia katika mabadiliko makubwa ya muundo wa AFC/M23, huku mapigano yakiendelea katika majimbo ya Kivu Kaskazini na Kivu Kusini.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, Joseph Kabila amekuwa akijitokeza kwa kiwango kikubwa zaidi katika mwelekeo wa kisiasa wa AFC/M23. Wachunguzi wa Umoja wa Mataifa wanasema Kabila ametembelea maeneo yanayodhibitiwa na muungano huo tangu Mei 2025 na kufanya mikutano na viongozi wake, jambo linalotafsiriwa kama ushahidi wa kuimarika kwa uhusiano wa kisiasa kati ya pande hizo.
Ripoti hiyo inanukuu vyanzo mbalimbali vinavyoeleza kuwa mazungumzo yanaendelea kuhusu kuufanyia AFC/M23 mageuzi makubwa ya kimuundo, ikiwa ni pamoja na uwezekano wa kutumia jina jipya. Hatua hizo zinaonekana kulenga kupanua mvuto wa kisiasa wa muungano huo huku zikidumisha azma yake ya muda mrefu katika mashariki mwa DRC.
Umoja wa Mataifa wakadiria AFC/M23 ina wapiganaji 30,000
Kundi la Wataalamu linakadiria kuwa AFC/M23 kwa sasa lina takribani wapiganaji 30,000, na hivyo kuwa moja ya makundi makubwa zaidi yenye silaha yanayofanya operesheni mashariki mwa DRC.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, nguvu hiyo inajumuisha wanajeshi wa zamani wa CNDP na waasi wa awali wa M23 wa mwaka 2012, waajiriwa wapya waliokusanywa tangu mwaka 2021 kutoka kwa diaspora ya Rwanda na kambi za wakimbizi, pamoja na maelfu ya waliokuwa wanajeshi wa Jeshi la DRC (FARDC), maafisa wa polisi na wapiganaji wa Wazalendo. Inaaminika wengi wa kundi hilo walijiunga na AFC/M23 baada ya kujisalimisha, kutoroka au kukamatwa kufuatia kuanguka kwa mji wa Goma.
Uwepo wa jeshi la Rwanda bado ni mkubwa
Ripoti hiyo inakadiria kuwa kati ya wanajeshi 14,000 na 18,000 wa Rwanda walikuwa wametumwa katika Kivu Kaskazini na Kivu Kusini kufikia mwishoni mwa Desemba 2025. Badala ya kuashiria kuondoka kwa majeshi hayo, wataalamu wanaamini harakati zilizoshuhudiwa baadaye zilikuwa ni mizunguko ya kawaida ya kubadilishana vikosi.
Ripoti inamtaja Jenerali Vincent Nyakarundi kuwa msimamizi mkuu wa operesheni hizo, huku Majenerali Eugene Nkubito na Vincent Gatama wakidaiwa kuongoza vikosi katika Kivu Kaskazini na Kivu Kusini, wakisaidiwa na vikosi maalumu vinavyoongozwa na Jenerali Stanislas Gashugi. Aidha, ripoti inamtaja aliyekuwa Jenerali James Kabarebe, ambaye sasa ni mshauri mwandamizi wa masuala ya ulinzi wa Rais Paul Kagame, kuwa afisa anayesimamia uratibu kati ya AFC/M23 na Joseph Kabila.
Ripoti hiyo pia inabainisha kuwa mamlaka za Rwanda hazikuwa zimejibu maombi ya Umoja wa Mataifa ya kutoa maoni kabla ya ripoti hiyo kuchapishwa.
Malengo yamebadilika kutoka kujiunga na FARDC hadi mfumo wa shirikisho
Kwa upande wa kisiasa, wataalamu wa Umoja wa Mataifa wanasema AFC/M23 haijitangazi tena kama kundi linalotaka kurejeshwa ndani ya Jeshi la Taifa la DRC (FARDC). Badala yake, sasa linapigania kuanzishwa kwa “Jamhuri ya Shirikisho la Congo” (Federal Republic of Congo) na linaeleza dhamira ya kuunda na kuongoza jeshi la shirikisho litakaloundwa chini ya mfumo huo.
Iwapo mabadiliko hayo ya kikatiba hayatatekelezeka, ripoti hiyo inaeleza kuwa AFC/M23 pia inafikiria uwezekano wa kuanzishwa kwa eneo lenye mamlaka ya kujitawala mashariki mwa DRC.
Pande zote zatuhumiwa kwa ukiukaji wa haki za binadamu
Ingawa ripoti hiyo inaitaja AFC/M23 kuwa mhusika mkuu wa ukiukaji wa haki za binadamu uliorekodiwa mwaka 2025, pia inalituhumu Jeshi la DRC (FARDC) kuwa mhusika wa pili kwa ukubwa, likihusishwa na matukio 789 yaliyorekodiwa.
Wataalamu hao pia wanadai kuwa serikali ya DRC iliwapa silaha wanamgambo wa Wazalendo kinyume na vikwazo vya Umoja wa Mataifa vya usambazaji wa silaha. Vilevile, wanaituhumu serikali hiyo kuendelea kushirikiana kioperesheni na FDLR, kundi lenye silaha lililowekewa vikwazo na Umoja wa Mataifa, licha ya ahadi za mara kwa mara za Kinshasa kulivunja.
AFC/M23 yajipanga kwa hatua mpya ya kisiasa
Mbali na kuelezea maendeleo ya kijeshi uwanjani, ripoti ya Umoja wa Mataifa inaonyesha kuwa AFC/M23 inaonekana kujiandaa kuingia katika awamu mpya ya kisiasa. Kuongezeka kwa uwezo wake wa kijeshi, malengo yake ya kufanya mabadiliko ya kikatiba, pamoja na uhusiano unaozidi kuwa wazi na Joseph Kabila, vinaashiria juhudi za kuibadilisha AFC/M23 kutoka muungano wa waasi wenye silaha na kuwa nguvu pana ya kisiasa, wakati vita vikiendelea kubadilisha mazingira ya usalama na siasa mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.
MENGINEYO
Kitabu Kipya: "A Spy's Guide to Deception" (Mwongozo wa Kijasusi Kuhusu Hadaa)
Baada ya miaka mingi ya kufanya kazi katika masuala ya ujasusi, usalama, uchambuzi wa kisiasa na ujasusi wa vyanzo vya wazi (OSINT), nimezindua rasmi kitabu changu kipya kinachoitwa “A Spy’s Guide to Deception” — hiki kikiwa kitabu cha kwanza katika mfululizo mpya wa vitabu uitwao



